Hili ndilo lililomkuta Agness Masogange tena, ahojiwa kwa zaidi ya saa 10 airport!

Kikosi Kazi cha Polisi cha Kuzuia Dawa za Kulevya nchini kimemhoji kwa zaidi ya saa 10, msanii Agnes Gerald ‘Masogange’ kuhusiana na tuhuma za kukamatwa na dawa aina ya crystal methamphetamine huko Afrika Kusini, Julai mwaka jana.




Kamanda wa Polisi Kitengo cha Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Gedfrey Nzowa alisema jana kuwa Masogange alianza kuhojiwa juzi usiku baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam akitokea Afrika Kusini.

Nzowa alisema baada ya kuhojiwa, Masogange aliruhusiwa na kwamba yupo huru, ameachiwa bila masharti yoyote.

Kamanda wa Polisi wa Uwanja wa Ndege, Hamisi Selemani naye alithibitisha kuhojiwa kwa msanii huyo akisema: “Hapa kuna kikosi kazi, kila mmoja alimhoji kwa wakati wake lakini kwa upande wa polisi tulimpekua na kumhoji lakini tumemwachia.”

Kamanda Selemani alisema Masogange alianza kuhojiwa juzi saa mbili usiku hadi jana saa nne asubuhi.

Hata hivyo, alipotakiwa kuzungumzia suala hilo, Masogange alikana akisema kwa kifupi na kukata simu: “Hilo unalosema siyo kweli na sipo tayari kuzungumzia hilo… Siwezi kuzungumza na chombo cha habari kwa sasa, shida yako nini?”

Masogange alitawala vyombo mbalimbali vya habari nchini katikati ya mwaka jana baada ya kukamatwa Afrika Kusini akiwa na nduguye Melisa Edward wakiwa na ‘mzigo’ wa dawa hizo zenye thamani zaidi ya Sh6.8 bilioni.

Wasichana hao walinaswa baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Oliver Tambo, Afrika Kusini wakitokea Tanzania.

Nzowa alisema jana kuwa katika mahojiano hayo walimuuliza kuhusiana na ushahidi alioutoa huko Afrika Kusini kuwa dawa hizo za kulevya alipewa na mtu kutoka JNIA. “Ni kweli tulikuwa tunamuhoji Masogange ili atueleze mtu gani aliyempa crystal methamphetamine kama alivyodai kuwa amepewa na mtu wa hapa JNIA,” alisema Nzowa.

Katika mahojiano hayo, Nzowa alidai kuwa Masogange alidai kuwa alipewa dawa hizo na mtu ambaye hamfahamu kwa jina lakini anaikumbuka sura yake. Alisema baadaye walikwenda eneo ambalo walipeana dawa hizo na mtu asiyemjua jina lake kwa ajili ya kuweza kumtambua kama alikuwapo eneo hilo.

Chanzo: MwananchI

Previous Post Next Post