WAUZA DAWA 462 KOTE NCHINI WAKUTWA NA VETI BANDIA!




Mwanza. Watu 462 kati ya 1,205 waliokuwa wakisailiwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kupitia Baraza la Famasi, wamebainika kuwa na vyeti bandia.
Kubainika huko kulijitokeza wakati wakifanyiwa mafunzo kuhusu uuzaji wa dawa katika maduka muhimu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Mwanza, Mratibu wa Mpango wa Maduka Muhimu katika Baraza la Wafamasi, Richard Silumbe, alisema Mkoa wa Mwanza, umeongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya watu waliobainika kuwa na vyeti bandia.
Kwa mujibu wa mratibu huyo, tatizo lilibainika wakati wa kutoa mafunzo elekezi kwa wanafanya kazi wa maduka ya dawa baridi, katika mikoa mbalimbali nchini.
“Asilimia 46 ya waliofika katika usaili huo, walikuwa na vyeti bandia kutoka katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando na vingine vikitoka katika Chuo cha Kanisa la AIC Korandoto. Hali hii imetutisha kwa sababu watu hawa wapo madukani na wanawahudumia wananchi,” alisema Kilumbe.
Alisema pamoja na kuwachuja wauguzi hao waliokuwa wameomba kupata mafunzo ya uuzaji wa maduka ya dawa muhimu, bado kuna wengine waliobainika kuwa hawana ujuzi wowote katika fani hiyo.
“Kati ya hao 1,205 waliofika katika usaili, 743 vyeti vyao vilikuwa havina shida lakini ulipokuja mtihani wengi wao walishindwa kujibu maswali hata yale ambayo hayahitaji mtu kuwa amesomea mambo ya afya walishindwa,” alisema Kilumbe.
Akieleza umuhimu wa kuwepo kwa maduka muhimu, alisema mpango huo umekuja kwa ajili ya kutoa huduma sahihi kwa wananchi tofauti na ilivyo sasa.
Alisema umuhimu huo ndiyo ulioifanya wizara kuamua kujiridhisha kuhusu watoa huduma hao kwa kuwapatia mafunzo ili waweze kutoa huduma za uhakika.
Alisema tayari mikoa yote imeishaanza kutekeleza mpango huo na kwamba Mwanza ndiyo ulikuwa mkoa wa mwisho.
“Hiyo imetokana na siasa za mkoa huo ambao wamiliki wengi wamekuwa wakipinga mpango huu kwa sababu zao binafsi,” alisema mratibu huyo.
Alisema biashara ya dawa ni nzuri kwa wafanyabiashara wanaofuata sheria.
Mfamasia wa Jiji la Mwanza, Edward Magelewanya, alisema zoezi hilo limekuwa na changamoto nyingi.
Previous Post Next Post

Popular Items