RAIS WA SOMALIA ATIMIZA MWAKA MMOJA MADARAKANI



Rais wa Somalia - Hassan Sheikh Mohamud

Baada ya mwaka wa kwanza madarakani kama rais wa taifa ambalo ni mahali pa hatari zaidi duniani na taifa lililoshindwa, Hassan Sheikh Mohamud bado anapambana na uwezo mdogo wa kifedha, rushwa,
Matatizo hayo ni pamoja na ukosefu wa utoaji huduma ,mauaji ya maafisa wa serikali nchini humo , ikiwa ni pamoja na jaribio dhidi ya maisha yake binafsi.(P.T)
Rais wa Somalia , ambaye jana Jumanne Septemba 10 alisherehekea siku 365 tangu alipochaguliwa kuwa rais na wabunge, amekuwa na wakati mgumu sana katika mwaka wake wa kwanza wa kipindi chake cha miaka minne ya uongozi.
Wadadisi wa masuala ya kisiasa wanasema kuwa sio tu kwamba Mohamud analazimika kupambana na makundi ya wapiganaji wa Kiislamu kama al-Shabaab , kundi ambalo limefanya mashambulio kadha hivi karibuni ya kigaidi katika mji mkuu Mogadishu licha ya kufurushwa kutoka miji kadha muhimu katika taifa hilo la pembe ya Afrika , na ongezeko la idadi ya majimbo yanayotaka kujitenga, pia anakabiliwa na hali inayoongezeka ya kukata tamaa miongoni mwa Wasomali.
Abdi Aynte , muasisi na mkurugenzi mtendaji wa taasisi ya turathi kwa ajili ya mitaala ya sera, (HIPS), taasisi ya kwanza nchini humo ya kubadilishana maarifa, amesema kuwa Mohamud ameshindwa kuleta matunda katika mwaka wake wa kwanza.
Sera ya nguzo sita
"Sera ya nguzo sita ilikuwa ya kutia moyo, lakini utoaji wa huduma kwa umma haukuwapo kabisa," Aynte ameliambia shirika la habari la IPS mjini Nairobi. Sera ya nguzo sita ilikuwa mkakati wa Mohamud wa kuleta usalama , uthabiti, haki , ufufuaji wa uchumi, na kutoa huduma kwa Somalia.
"Kwa hiyo hakuna cha ajabu kwamba hatuna maendeleo yanayoonekana yaliyofikiwa kuelekea kutimiza hata moja kati ya nguvu hizo."
Wasomali wamekimbia makaazi yao baada ya ghasia
Wasomali wameishi kwa karibu miaka 20 katika vita , umasikini na kutawanyika kufuatia kuondolewa madarakani dikteta na rais wa zamani Mohamed Siad Barre mwaka 1991. Nchi hiyo haijakuwa na serikali kuu hadi mwaka 2000, baada ya kuwa na serikali kadha za mpito ambazo zilichaguliwa.
Pia kuna huduma muhimu chache ama vituo vya huduma za afya vichache nchini humo , huduma nyingi hata hivyo zikitolewa na mashirika yasiyo ya kiserikali. Kwa muda wa miaka 20 shirika la madaktari wasio na mipaka , Medecins Sans Frontieres, lilikuwa moja kati ya watoaji wachache wa huduma ya afya ya msingi nchini Somalia.
Lakini mwezi Agosti shirika hilo lilijitoa kutoka nchini humo baada ya kuuwawa na kusumbuliwa kwa wafanyakazi wake kila mara na kufanya kuwa vigumu kwa shirika hilo kufanyakazi nchini humo.
Lakini wasaidizi wa Mohamud wamekuwa wepesi kumtetea profesa huyo wa zamani na mwanaharakati wa vyama vya kijamii, ambaye alinusurika katika jaribio la kuuawa wakati akisafiri kwenda katika mji wa kusini nchini humo wa Merca hapo Septemba 3.
Matatizo ya kifedha
Msemaji wa rais Abdirahman Omar Osman ameliambia shirika la habari la IPS kuwa nchi hiyo ina matatizo makubwa ya kifedha ambayo yanafanya kuwa vigumu kwa Mohamud kuweza kutimiza ahadi zake.
"Serikali haina fedha za kutosha kufanya kila kitu," Osman ameliambia shirika hilo la IPS mjini Mogadishu.
Njaa na magonjwa nchini Somalia
"Mapato ya serikali ya kila mwezi ni wastani wa dola milioni tatu kutokana na bandari ya Mogadishu na uwanja wa ndege, wakati huo huo bajeti inayohitajika kutekeleza shughuli za kawaida za kila siku ni kiasi cha dola milioni 20 kila mwezi," amesema.
Hata hivyo, tarakimu zilizotolewa na Osman zinapingana na zile alizotoa naibu mkurugenzi mkuu wa bandari ya Mogadishu Abdiqani Osman Kabareto. Kabareto ameimbia redio moja nchini humo ya Ergo mwezi August kuwa bandari ya mjini Mogadishu inauwezo wa kuzalisha kiasi cha kati ya dola milioni nne na tano kila mwezi.
"Fikiria serikali ikiwa na uhaba wa aina hiyo wa bajeti ikijaribu kujenga na kuunda taasisi kutoka mwanzo kabisa . Hapa ndio penye tatizo. Sio kwamba serikali haiko tayari, ni matatizo ya upungufu wa fedha," amesema Osman.
Mohammed Ali , mhitimu wa chuo kikuu cha Somad , ambacho Mohamud alisaidia kukiasisi, ameliambia shirika hilo la IPS kuwa licha ya kuwa aliunga mkono kuchaguliwa kwa Mohamud , anahisi kuwa hakuna cha kufurahia baada ya mwaka mmoja madarakani.
Previous Post Next Post

Popular Items