TANZANIA YATAKA BARAZA KUU LA USALAMA KUUNGA MKONO JUHUDI ZA KULETA AMANI YA KUDUMU DRC


540793 9fd59
Na: Mwandishi Maalum
Tanzania  imelitaka  Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa  kuendelea kuunga mkono mikakati na juhudi mbalimbali zinazolenga katika kurejesha amani ya kudumu katika eneo la  Mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Wito  huo umetolewa na  Mhe. Tuvako Manongi,Balozi wa  Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa  Tanzania katika Umoja wa Mataifa. Alikuwa akichangia majadiliano ya...
wazi kuhusu operesheni za kulinda amani,  ujenzi wa amani na maendeleo. Majadaliano hayo yamefanyika siku ya  jumatatu na kufunguliwa na  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki  Moon,  na yaliandaliwa na Pakistani, nchi ambayo ni Rais wa Baraza hilo kwa mwezi huu wa Januari.
Katika mchango wake,   Tanzania kupitia  Mwakilishi  wake  , imeeleza  bayana kuwa, hali  iliyojitokeza mwezi Novemba mwaka jana huko Goma, ni kielelezo na ushuhuda wa dhahiri kwamba juhudi na mikakati mbadala ya  ulinzi wa amani inahitajika katika  kuwakabili  wavurugaji wa amani katika eneo hilo.
 “Ni muhimu sana kwa Baraza hili likaendelea kuunga mkono uwepo wa uwajibikaji mkubwa zaidi katika suala zima la  operesheni ya kulinda amani katika DRC. Tulichokishuhudia Goma mwezi Novemba mwaka jana,  ni kilelezo cha dhahiri   cha kutakiwa  kuwepo kwa vikosi vya kulinda amani vyenye    dhamana kubwa  na uwajibikaji zaidi katika kuwakabili na kuwadhibiti wavurugaji amani” akasema Balozi Manongi.
Balozi Tuvako Manongi amesisitiza  ili amani ya kudumu iwepo nchini DRC, na hususani eneo hilo la Mashariki,  panahitajika pia uwepo wa vikosi vya ulinzi wa amani vitakavyokuwa na uwezo wa   kuchukua maamuzi  ya haraka  na wakati mwingine katika mazingira magumu kama sehemu muhimu ya kuchagiza ufanisi na mafanikio.
Akabainisha kwamba vikosi  hivyo lazima viwe na uwezo wa  kutegemewa na raia vinavyopaswa kuwalinda , na ikibidi kuwapiga ipasavyo wale wanaotaka kuendelea kuhatarisha maisha ya raia wasio na hatia. 
Mwakilishi  huo wa Tanzania, akaeleza zaidi kwamba  vitendo vya kikatili ambavyo vimekuwa vikifanywa na  makundi yenye silaha  dhidi ya raia   , ni ukumbusho mwingine  wa  kuhitajika kwa  juhudi za pamoja za kutafuta amani ya kudumu katika eneo hilo.
Aidha Balozi Manongi amesisitiza kwamba ni jambo la muhimu sana kwa Umoja wa Mataifa na Taasisi za Kikanda kugawana majukumu linapokuja suala la ulinzi.
Amelihakishia Baraza  kwamba  katika suala hilo la  DRC, litapata ushirikiano mkubwa kutoka  Umoja wa Afrika ( AU), Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi  za  Kusini mwa Afrika ( SADC) na Mkutano wa Kimataifa kuhusu Eneo la Maziwa Makuu ( ICGLR).
Vilevile Balozi  akabainisha wazi kwamba,  kwa kushirikiana na taasisi za kikanda,Umoja wa Mataifa haupashwi kuhofia  kupoteza wajibu wake  wa msingi katika  ulinzi wa amani bali ushirikiano huo unalenga katika kuleta tija na mafanikio.
Majadiliano  hayo yalitanguliwa na wajumbe 15 wa Baraza Kuu la Usalama kupisha kwa kauli moja Azimio namba2086 ( 2013). Azimio hilo la kwanza la aina yake kupitishwa katika kipindi cha miaka kumi iliyopita linatambua na kuidhinisha kwamba suala la  ulinzi wa amani linahitaji kushughulikiwa kwa njia au mifumo mbalimbali.
Aidha azimio hilo  pamoja na masuala mengine, linasisitiza kwamba operesheni za kulinda amani lazima zifanyike katika namna ambayo itahusisha ulinzi wa amani,  kuzuia kujirudia kwa migogoro na vita , kusaidia katika ujenzi wa amani endelevu , maendeleo endelevu, ujenzi wa demokrasia, utawala shirikishi na uundwaji  taasisi zinazounda mfumo mzima wa serikali.
Previous Post Next Post